emblem

Mamlaka ya Serikali Mtandao

Uadilifu na Ubunifu kwa Utoaji Huduma Bora kwa Umma
TAASISI YENYE VIWANGO VYA ISO 9001: 2015

TAASISI NA HALMASHAURI ZAENDELEA KUNEEMEKA NA MFUMO WA e-BOARD


TAASISI NA HALMASHAURI ZAENDELEA KUNEEMEKA NA MFUMO WA e-BOARD


Taasisi na Halmashauri mbalimbali nchini zimeendelea kuunganishwa na kunufaika na matunda ya ubunifu ya wataalamu wa ndani yatokanayo na mfumo wa e-Board.

Uanzishwaji wa mfumo huu ni Juhudi za Serikali kupitia Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) za kuhakikisha matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yanaimarishwa ili kuboresha utendaji kazi wa Taasisi za Umma nchini.

Mfumo wa eBoard ni mfumo unaoratibu vikao vya Bodi, Kamati za Bodi na Menejimenti kwa kuruhusu kuandaa kikao, kutengeneza dondoo na muktasari (minutes) kwa lengo la kutunza kumbukumbu za kikao husika.

Mchambuzi wa Mifumo ya TEHAMA kutoka eGA Caesar Mwambani anasema kwamba lengo la uanzishwaji wa mfumo huu lilikuwa ni kuwezesha utendaji kazi wa bodi za Taasisi mbalimbali kuwa na rejea za vikao.

“Awali ulianza kutumika kwa ajili ya vikao vya bodi tu, lakini baada ya mahitaji kuongezeka tuliona ni vyema tupanue mawanda ya matumizi yake ili menejimenti ya Taasisi husika pia iweze kutumia mfumo huu.” Amefafanua.

Aidha, pamoja na uwezo wa kutunza kumbukumbu za vikao, mfumo huu unawaruhusu wajumbe wa bodi kupiga kura kunapokuwa na maamuzi yanayohitaji wajumbe kupiga kura na hivyo kurahisha utoaji wa maamuzi utakaochochea utoaji wa huduma kwa haraka zaidi kwa wananchi.

Mfumo huu pia umekua suluhu kubwa katika kupunguza gharama za utendaji kazi kwenye eneo hili la vikao ndani ya Taasisi za Umma.

Mpaka sasa Taasisi za Umma takribani 20 zimeunganishwa kwenye mfumo huu ikiwemo Tume ya Ushindani Tanzania (FCC), Mfuko wa Bima ya Taifa (NHIF), Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA), Halmashauri ya Wilaya Ilemela, Muleba na nyinginezo.

Pia mfumo huu umeunganishwa na mfumo wa e-Mikutano hivyo washiriki wanaweza kuunganishwa katika jukwaa moja ili kujadiliana mambo mbalimbali ya maendeleo ya Taasisi.