emblem

Mamlaka ya Serikali Mtandao

Uadilifu na Ubunifu kwa Utoaji Huduma Bora kwa Umma
TAASISI YENYE VIWANGO VYA ISO 9001: 2015

UTUMISHI YATEKELEZA MAELEKEZO YA MHE. RAIS KUUNDA MFUMO WA KIELEKTRONIKI WA KUSHUGHULIKIA MALALAMIKO YA WANANCHI


UTUMISHI YATEKELEZA MAELEKEZO YA MHE. RAIS KUUNDA MFUMO WA KIELEKTRONIKI WA KUSHUGHULIKIA MALALAMIKO YA WANANCHI


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama amesema, ofisi yake kwa kushirikiana na Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) imetekeleza maelekezo ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ya kusanifu Mfumo wa kielektroniki wa kupokea, kufuatilia na kushughulikia malalamiko (e-Mrejesho) ambao utatoa fursa kwa wananchi na wadau kuwasilisha malalamiko, maoni, mapendekezo, maulizo na pongezi Serikalini.

Mhe. Jenista amesema hayo jijini Dodoma wakati akifungua mafunzo ya matumizi na uendeshaji wa mfumo wa kutuma, kupokea na kufuatilia malalamiko, mapendekezo, maulizo na pongezi (e-Mrejesho) yaliyotolewa kwa Maafisa Malalamiko na TEHAMA wa Sekretarieti za Mikoa, Mamlaka za Serikali za Mitaa, Wizara, Wakala na Idara Zinazojitegemea ambao wamepewa dhamana na taasisi zao kushughulikia malalamiko.

Mhe. Jenista amesema kuwa, mfumo huo wa kielektroniki uliosanifiwa na wataalam wazawa ni rafiki kwa wananchi na Watumishi wa Umma kuutumia, hivyo utakuwa ni mkombozi kwa Watanzania katika kuwasilisha malalamiko kwa wakati ili yafanyiwe kazi na Serikali.

“Ni mfumo ambao unatoa mrejesho kwa Watumishi wa Umma na wananchi kuhusu huduma zote zinazotolewa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia taasisi zake,” Mhe. Jenista amesisitiza.

Sanjari na hilo, Mhe. Jenista amesema kuwa, licha ya mfumo huo kutoa taswira ya utendaji kazi wa Serikali, pia unatoa fursa kwa wananchi kutoa pongezi kwa Serikali, iwapo imefanya jambo jema lenye tija kwa taifa ili jambo hilo liendelezwe kwa manufaa ya umma.

Mhe. Jenista ameongeza kuwa, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan inasisitiza sana ushughulikiaji wa malalamiko ya wananchi kwa wakati katika taasisi zote za Umma, hivyo taasisi zote za umma zinapaswa kutoa kipaumbele cha kuutumia mfumo huo wa kielektroniki kushughulikia malalamiko ya wananchi yanayowasiliswa katika taasisi zao.